Kahama.
Chama kikuu cha ushirika cha Kahama KACU LTD kimesaini mkataba wa makubaliano na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) na Benki ya CRDB kurahisisha upatikanaji wa bima ya afya kwa wakulima ambapo ushirikiano huo utawawezesha wakulima kupata bima ya afya za NHIF kwa mkopo. Huduma hiyo ambayo imepewa jina la “Ushirika Afya Premium Loan” itatolewa kwa wakulima ambao wapo katika vyama vya ushirika huku pia ikiwanufaisha wategemezi wao, kwa maaana ya mke/ mume na watoto.
Hafla ya utiaji saini mkataba huo wa makubaliano imefanyika Wilayani Kahama katika ofisi za Chama kikuu cha Ushirika KACU LTD.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa biashara wa Benki ya CRDB, Dr. Joseph WIHS amesema katika makubaliano hayo Benki ya CRDB itakuwa ikisaidia kulipa gharama za bima ya afya (premium) na wakulima kulipa mwisho wa msimu baada ya kuuza mazao yao.
“Mkopo utatolewa kulingana na kiwango cha gharama za malipo ya bima ya afya (premium) ambapo kwa mtu mzima ni shilingi 76,800 na mtoto shilingi 50,400,” aliongezea Dr Joseph huku akibainisha kuwa mkopo huo wa bima ya afya utatolewa bure bila ya makato wala riba yoyote.
Kupitia huduma hiyo ya “Ushirika Afya Premium Loan”, Mkulima pia anaweza kuchukua kifurushi cha familia cha malipo ya shilingi 355,200 ambapo atapata bima ya afya kwa watu 6 (watu wazima 2, watoto 4). Kifurushi hiki kimeanzishwa ili kuhamasisha wakulima kukata bima kwa familia zao.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugezi wa huduma kwa wateja NHIF, Hipoliti Lello, amesema kuwa, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya umejipanga kuhakikisha unawahudumia kikamilifu wakulima ili wawe na uhakika na shughuli zao za kilimo katika kipindi chote cha mwaka.
“Lengo kubwa la mpango huu ni kuwawezesha wakulima wawe na uhakika wa afya zao kwa maana ya kupata huduma za matibabu wakati wowote wanapozihitaji na kwa upande wa Mfuko tumeboresha zaidi huduma zetu ili mwanachama wetu asipate usumbufu wa aina yoyote,” amesema Lello.
Akizungumza kwenye uzinduzi wa mpango huu, Kaimu Mrajis Msaidizi wa Vyama vya ushirika wa Mkoa wa SHinyanga Bi Hilda Boniphace amezipongeza CRDB na NHIF kwa kuwajali wakulima na kuwapatia uhakika wa matibabu wakati wote kupitia “Ushirika Afya Premium Loan”
Mwenyekiti wa chama kikuu cha ushirika cha Kahama Bw. Emmanuel P Cherehani mfuko wa bima ya afya NHIF na benki ya CRDB kwa kuja na mpango huu wa kuwasaidia wakulima “KACU LTD ipo tayari kushirikiana na Wadau wenye nia njema ya kuendeleza Wanaushirika katika nyanja mbalimbali za maendeleo ikiwemo afya na nyinginezo. Tutashirikiana na yeyote mwenye dhamira ya kweli kumnufaisha Mwanaushirika na mkulima kwa ujumla” amesema Bw. Cherehani.
MWISHO
